Meya wa Ubungo, Boniphace Jacob amesema Jumanne wiki ijayo atafungua kesi ya jinai dhidi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kutokana na madai ya kuwa na vyeti feki.
 
Jacob pia amesema, atamshtaki Makonda katika sekretarieti ya maadili ya utumishi wa umma, tume ya haki za binadamu pamoja na utawala bora.
 
Jacob ameeleza kuwa kesi hiyo itasimamiwa na mawakili maarufu Tundu Lissu ambaye ni Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA na Peter Kibatala..

Kesi hiyo itafunguliwa wiki ijayo baada mawakili hao kumaliza mchakato wa uchaguzi wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS) unaotarajiwa kufanyika Jumamosi Machi 18 mwaka huu ambapo Tundu Lissu ni mmoja wa wagombea wa kiti cha urais 
 
 
 

Serikali yapiga marufuku kufunga ndoa bila cheti cha kuzaliwa

SeeBait
Serikali  imepiga marufuku watu kufunga ndoa bila kuwa na cheti cha kuzaliwa kuanzia Mei Mosi, mwaka huu.

Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Harrison Mwakyembe amesema hayo leo akiwa katika ziara yake mkoani Morogoro na kuongeza kuwa serikali imeamua kufanya hivyo ili kupata takwimu sahihi za wananchi wake zitakazosaidia kupanga mipango ya kimaendeleo sanjari na kuzuia wageni kuingia kinyemela nchini.

Pamoja na mambo mengine, Dk.Mwakyembe amewataka Wakala wa Usajili wa vizazi na Vifo (RITA), kuhakikisha inasimamia sheria ya usajili ambapo amesema kuwa bila kuwa na  takwimu sahihi  za  vizazi na vifo ama ndoa  inasababisha nchi kushindwa kusonga mbele kimaendeleo.

“Wenzetu nchi zilizoendelea suala la usajili wamelipa kipaumbele lakini sisi bado tuko nyuma, kwa mfano Mkoa wa Morogoro  kwa mujibu wa sensa  ya watu na makazi ya mwaka 2012, inaonyesha kuna jumla ya wakazi milioni 2.2, lakini waliosajiliwa na kuwa na vyeti  vya kuzaliwa ni asilimia 11 pekee huku wengine wakiwa bado hawasajiliwa,” amesema.

Dk. Mwakyembe pia ametumia nafasi hiyo kuwaonya watendaji wa mahakama watakaolalamikiwa na wananchi kufanya kazi kinyume na maadili ikiwamo upokeaji wa rushwa ama kutotenda haki na kutumia  mahakama kugeuza kesi za madai kuwa kesi za jinai.
 
 
 
 
 

Rais Magufuli atembelea eneo la ujenzi wa Ikulu Chamwino Dodoma na kufyatua matofali

SeeBait
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 16 Machi, 2017 ametembelea eneo la ujenzi wa Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma na kuwahakikishia wananchi kuwaatahamia Dodoma hivi karibuni kama alivyoahidi.

Mhe. Rais Magufuli ambaye ameongozana na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenister Joakim Mhagama na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi John Kijazi amesema pamoja na majengo ya Ikulu Serikali itajenga miundombinu mingine zikiwemo reli na barabara za lami zitakazounganisha maeneo ya vijiji vinavyozunguka Ikulu na mji wa Serikali.

Pia Mhe. Dkt. Magufuli amewahakikishia wananchi kuwa wote watakaoguswa na shughuli za ujenzi wa miundombinu ya Serikali na wanaostahili kulipwa fidia watalipwa, na ametoa wito kwa wananchi hao kutumia fedha za fidia watakazolipwa kujenga makazi bora na kujipanga kufanya shughuli zenye manufaa kwao.

“Hapa sasa watakuja watu wengi, wafanyakazi na wageni maana tayari Mabalozi wa nchi mbalimbali nao watajenga ofisi zao hapa, sasa na nyinyi mjipange kufanya biashara, mtapata soko la kuuza mazao na bidhaa nyingine, mkipata fedha ziwasaidie kwa manufaa na sio kuzichezea” amesisitiza Mhe. Rais Magufuli.

Kwa upande wake Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa amesema utekelezaji wa Serikali kuhamia Dodoma unakwenda vizuri ambapo mpaka sasa viongozi wakuu wa wizara zote na wafanyakazi 2,069 wameshahamia Dodoma na wengine wanaendelea kuhamia Dodoma.

Mhe. Majaliwa ameongeza kuwa atasimamia utekelezaji wa maagizo ya Mhe. Rais Magufuli aliyeagiza kujengwa kwa reli itakayounganisha eneo la Bwigili na Dodoma mjini ili kurahisisha usafiri wa watu pamoja na kuharakisha ujenzi wa barabara za kuzunguka mji wa Dodoma na barabara za kuunganisha mji wa Serikali na Dodoma Mjini.

Wakiwa katika eneo hilo, Mhe. Rais Magufuli na Waziri Mkuu Mhe. Majaliwa wameshiriki ufyatuaji wa matofali yatakayotumia katika ujenzi wa majengo ya Ikulu.

Mapema kabla ya kutembelea eneo hilo, Mhe. Rais Magufuli amepokea taarifa ya mapendekezo ya ujenzi wa Mji wa Serikali wa Makao Makuu Dodoma kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Mhandisi Paskasi Muragili na kuagiza ujenzi wa Mji huo uzingatie maslai ya Taifa.

 
 

Post a Comment

 
Top